Naibu Waziri Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu |
Naibu Waziri Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, alisema hayo wakati wa kikao cha wadau wa ulinzi wa maliasili na utalii, ambacho pamoja na mambo mengine kimekutana kujadili wimbi la ujangili wa tembo katika hifadhi zilizopo mikoa ya Nyanda za Juu Kusini.
Alisema mpango huo wa kuwaumbua baadhi ya watu wanaofadhili ujangili ama kusafirisha meno ya tembo kwenda nchi za Kiarabu na China, utakolezwa na mbinu mpya za kiintelijensia ambazo zitatumika katika ‘Operesheni Uhai’ ambayo inatarajiwa kuanza hivi karibuni.
“Wanaofadhili shughuli za ujangili tutawatangaza majina yao hadharani katika kukabiliana na tatizo hili. Lakini pia wageni wote watakaokamatwa nchini kutokana na ujangili tutawafukuza ndani ya saa 24 tena watapaswa kulipa nauli za ndege kwa gharama zao baada ya kutumikia adhabu watakazopata kwa mujibu wa sheria,” alisema Nyalandu.
Alisema hivi sasa wimbi la ujangili nchini limekuwa kubwa kutokana na majangili hao kudaiwa kusaidiwa na baadhi ya wafanyakazi walioko kwenye vitengo vya ulinzi na usalama kwa kuwa suala zima la usafirishaji wa pembe za ndovu hauwezi kuvuka kwenye mikoa husika pamoja na hifadhi zetu hadi kwenda bandarini wasikamatwe au kufahamika kama baadhi ya watendaji hawausiki.
Alisema ujangili wa tembo unaongezeka kila mwaka na kwamba hali hiyo inahusisha mtandao mkubwa wakiwepo wafanyakazi wanaozunguka maeneo hayo, ambapo inasemekana kuwa kila mwaka tembo 10,000 wanauawa, kitu ambacho kinahatarisha usalama wa tembo hao kuendelea kuwepo.
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa), Dk. Allani Kijazi, alisema katika kukabiliana na ujangili kwenye mikoa ya Iringa, Njombe, Mbeya na Dodoma, wadau wataunda kikosi kazi ambacho kitapambana na ujangili hasa katika hifadhi ikiwemo Ruaha ambayo kwa sasa ndiyo hifadhi kubwa nchini.
CHANZO:
NIPASHE
0 comments:
Post a Comment