|
Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) ambaye pia ni Mhariri
Mtendaji wa New Habari (2006), Absalom Kibanda, akizungumza na
waandishi wa habari katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa |
Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Absalom Kibanda,
amerejea nchini kutoka Afrika Kusini alikokwenda kutibiwa, huku akiwa na
siri moyoni kuhusu kilicho nyuma ya matukio mabaya yaliyowasibu baadhi
ya waandishi wa habari, akiwamo yeye, ambayo ameahidi kuisema iwapo
Mungu atampa uzima.
Alisema atafanya hivyo ili kuliokoa taifa, wanahabari wenzake na
Watanzania kwa jumla, ili kuwasaidia wasiingie kwenye madhila, maumivu
na mateso kama yale yaliyompata.
Kibanda ambaye pia ni Mhariri Mtendaji wa Kampuni ya New Habari 2006
Limited, aliwasili nchini jana saa 7.55 mchana, akitokea Hospitali ya
Milpark nchini humo, ambako alilazwa kwa miezi mitatu kisha kukaa
hotelini kwa muda, baada ya kuvamiwa na watu wasiojulikana wakati
akirejea nyumbani kwake, Mbezi Juu, jijini Dar es Salaam, Machi 5, mwaka
huu.
Katika tukio hilo, watu hao walimng’oa meno, kumkata kidole, kumjeruhi kwa kitu kizito kichwani na kumharibu jicho la kushoto.
Baada ya tukio hilo, Machi 6, mwaka huu, Kibanda alilazwa katika
Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) na baadaye katika Taasisi ya Tiba ya
Mifupa (MOI), jijini Dar es Salaam.
Kisha alipelekwa Afrika Kusini na kulazwa katika Hospitali ya Milpark, jijini Johannesburg.
Kibanda alisema hayo alipozungumza na waandishi wa habari muda mfupi
baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere
(JNIA) jijini Dar es Salaam jana na kupata mapokezi makubwa kutoka kwa
mamia ya wakazi wa Dar es Salaam, wakiwamo wahariri, waandishi na
wananchi wengine.
Alisema akiwa Afrika Kusini, alipata taarifa nyingi kuhusiana na tukio lake na mengine yaliyowasibu wanahabari wengine nchini.
Kibanda alisema hataki kufanya makosa ya watu wengine na kwamba, yeye mwenyewe anakusudia kuyasemea hayo kila wakati.
“Katika matukio yangu na mengine, kama Mungu atanipa uzima nitalisemea. Tumekuwa tukipata taarifa nyingi,” alisema Kibanda.
Alisema alipouawa mwandishi wa habari aliyekuwa mwakilishi wa kituo cha
televisheni ya Channel Ten, mkoani Iringa, marehemu Daud Mwangosi,
alishiriki katika kutoa tamko la TEF lililokuwa la pamoja na Baraza la
Habari Tanzania (MCT).
Pia alishiriki katika kufuatilia matukio mbalimbali ya waandishi
kuumizwa au kujeruhiwa, likiwamo lile lililomsibu Shaban Matutu
(Tanzania Daima) na Mnaku Mbani (Business Times).
“Nataka kuwahakikishia wanahabari wenzangu, kwamba, matukio yote haya si ya bahati mbaya,” alisema Kibanda.
Alisema wakati akiyapitia na kuyaangalia matukio ya wanahabari wenzake,
hakujua hata siku moja kwamba, pengine na yeye kama angefikwa na matukio
hayo.
“Nawaomba wanahabari wenzangu tufanye lolote tunaloweza kuhakikisha
tukio la Kibanda linakuwa la mwisho. Matukio ya watu kupanga njama au
kula njama na kujeruhi watu,” alisema Kibanda.
Kibanda alisema tukio la kutekwa, kuteswa na kujeruhiwa kwa aliyekuwa
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari Tanzania, Dk. Stephen Ulimboka,
linafanana sana kimazingira na kimkakati na tukio lake.
Kibanda alisema akiwa hospitali Afrika Kusini, serikali ilituma
mpelelezi, ambaye ni afisa wa ngazi za juu wa Jeshi la Polisi kuzungumza
naye juu ya janga lililomkuta.
Pia alisema hataki kabisa kuwa mbinafsi kwa sababu anajua kwamba, mpaka
sasa wanahabari na Watanzania kwa jumla wanashuhudia ukimya miongoni mwa
vyombo mbalimbali vya dola unaoendelea kuhusu hatima ya uchunguzi wa
tukio lake.
Kibanda alisema kinyume cha ukimya huo, vyombo hivyo viliahidi kwamba,
vitalifanyia kazi tukio lake kwa kina na hatimaye watu waliohusika
kufikishwa mbele ya mkono wa sheria.
Alisema kabla hajaondoka hospitali, alitembelewa na Mkuu wa Jeshi la
Polisi nchini, Inspekta Jenerali (IGP), Said Mwema, na Kamanda wa Polisi
Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Naibu Kamishna (ACP) Suleiman Kova.
Kwa mujibu wa Kibanda, ahadi ya kulifanyia kazi tukio lake alipewa na
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi, alipomtembelea
hospitali Afrika Kusini, kwamba serikali itafanya lolote inaloweza.
“Bado namuuliza Mungu kwanini aliruhusu niwe hai hadi leo? Kama kuna
ujumbe wa uhai wangu leo nina wajibu ninaotaka kuutimiza ili kuliokoa
taifa langu, wanahabari wenzangu na Watanzania wengine wasiingie katika
madhila, maumivu na mateso makali, ambayo nimepata,” alisema Kibanda.
Alisema ana kila sababu ya kufanya jambo, ambalo litawatoa Watanzania hapa walipo sasa.
“Kwa sababu hiyo nasema ndugu zangu, msimlilie Absalom Kibanda. Ililieni
nchi yetu, ambayo katika kipindi cha miaka karibu nane ya utawala wa
awamu nne, matukio ya namna hii yanaendelea kushamiri na hakuna
linalofanyika,” alisema Kibanda.
Alisema akiwa Afrika Kusini, alisoma taarifa na kusikia kauli mbalimbali
kutoka kwa wanasiasa, wanahabari na watu wengine kuhusu tukio lake.
Kibanda alisema la mwisho alilolisoma lilikuwa ni tamko la TEF, ambalo
alisema walifanya kazi kubwa, ikiwa ni pamoja na kuandika muhtasari
mzito sana.
Alisema zaidi ya hivyo, TEF walisafiri kwenda Afrika Kusini kuzungumza
naye ingawa wakati huo alikuwa na maumivu makali kulinganisha na hivi
sasa, lakini walifanikisha kazi yao na matokeo ameyaona.
Kibanda alisema: "Kama utasoma ripoti ya TEF, utagundua kwamba, kuna mambo mengi yaliyo nyuma ya ripoti hiyo."
Kabla ya kuanza kuzungumza hayo, Kibanda alibubujikwa machozi baada ya
kushuhudia umati mkubwa wa watu waliofika uwanjani hapo kumpokea.
Baadhi wanahabari walibeba mabango yenye ujumbe wa kumkaribisha nyumbani
na kuvihoji vyombo vya dola kuhusu hatima ya uchunguzi wa tukio lake.
Kibanda alisema ametoa machozi kwa sababu ya mshikamano mkubwa aliouona jana katika mapokezi yake.
Aliwashukuru wahariri, wanahabari, vyombo vyote vya habari na Watanzania
kwa jumla kwa moyo wa ushirikiano na mshikamano waliouonyesha kufuatia
matukio yaliyomsibu.
Pia alimshukuru Mwenyekiti wa Chama Wamiliki wa Vyombo vya Habari
Tanzania (Moat), ambaye pia ni Mwenyekiti Mtendaji wa IPP, Dk. Reginald
Mengi, kwa msaada mkubwa alioutoa kwake.
Alisema bado ana maumivu ya mwili, lakini hana maumivu ya roho na
kuwaambia wanahabari na Watanzania kwamba, wana wajibu wa kuliokoa taifa
kwani limepita katika kipindi kigumu.