Home » » Twanga kusherehekea miaka 15

Twanga kusherehekea miaka 15

mkurugenzi wa bendi ya muziki wa dansi ya African Stars 'Twanga Pepeta', Asha Baraka
Bendi ya muziki wa dansi ya African Stars 'Twanga Pepeta' inatarajia kufanya onyesho la sherehe za kutimiza miaka 15 ya bendi hiyo pamoja na uzinduzi wa albamu mpya ya bendi hiyo iitwayo 'Nyumbani ni Nyumbani' Juni 30 mwaka huu kwenye viwanja vya Leaders Club, Kinondoni jijini Dar es Salaam.

Akizungumza jana jijini, mkurugenzi wa bendi hiyo, Asha Baraka, alisema kuwa maandalizi ya sherehe hizo yanaendelea vyema na kwamba kabla ya kuzindua albamu hiyo ya 12 usiku, asubuhi kutakuwa na shughuli mbalimbali za michezo zitakazowahusisha wadau na wapenzi wa bendi hiyo.

Asha alisema kuwa ndani ya miaka 15 ya kuwapo kwa bendi hiyo wamekumbana na changamoto mbalimbali ambazo zimemsaidia kuiimarisha na kubaki kwenye soko la muziki.

Alisema pia siku ya uzinduzi huo wanatarajia kuuza CD za albamu yao ya 11 iliyozinduliwa mwaka jana lakini mauzo yake yalisimama kufuatia kukamatwa kwa CD bandia siku moja baada ya uzinduzi.

"Tunatarajia kuwa na ujio tofauti katika uzinduzi na sherehe za miaka 15, pia napenda kuwaambia wapenzi wa muziki wa dansi kuwa muziki huu haujashuka ila haujapata nafasi ya kutangazwa, tunawaomba wamiliki wa vituo vya redio na televisheni watusaidie kwani bila kuonekana au kusikika muziki hauwezi kukua," alisema Asha.

Alisema uzinduzi wa albamu ya 'Fainali Uzeeni' iliyobebwa na wimbo huo uliotungwa na Jesca Charles, kuwa ndiyo uliovunja rekodi kwa onyesho lake kuhudhuriwa na mashabiki wengi na vile vile albamu hiyo kuuza nakala nyingi.

Alieleza kwamba suala la wanamuziki kuhama na kurejea katika bendi hiyo kwake halimsumbui na anajivunia kwa sababu wanamuziki wake wanafuatwa kutokana na wao kupika wanamuziki bora na kazi hiyo ndiyo wanaendelea kuifanya.

Wakati huo huo, Asha jana alitangaza kuzindua rasmi kwa studio mpya ya kurekodi nyimbo za muziki na filamu iitwayo Flavour Inc iliyopo jijini Dar es Salaam.

Alisema studio hiyo iliyoko chini ya mtayarishaji, Yunick Bulla 'Awax', itakuwa inarekodi nyimbo za aina mbalimbali na lengo lake ni kuwapa nafasi wasanii chipukizi kutengeneza kazi zao kwa gharama nafuu na vile vile kuwasaidia kuzitangaza kazi hiyo.

0 comments:

Post a Comment

Blog Archive

Popular Posts

.

CHAT BOX

My Blog List

 
Support : BONGOCLANTZ
Copyright © 2013. KANGAROO - All Rights Reserved
Template Created by EDDIE SUCRE
Proudly powered by Blogger