Home » » Mwili wa Ngwair kutua leo saa 8

Mwili wa Ngwair kutua leo saa 8

Albert Mwangweha a.k.a Ngwair
Mwili wa msanii Albert Mwangweha a.k.a Ngwair unatarajia kuingia nchini leo majira ya saa 8 mchana kwa ndege ya Shirika la Afrika Kusini (South Africa Airways).

Akizungumza na NIPASHE jana msemaji wa Kamati ya Mazishi, Adam Juma alisema kibali cha kifo cha msanii huyo tayari kimekamilika na akawashukuru wote waliowezesha mwili huo kuwasili.

"Kila kitu kipo sawa na tunamshukuru Mungu kwa kweli kwamba sasa ndugu yetu atawasili nchini tayari kwa kuzikwa, ni jambo la heri kwa kweli," alisema Adam.

Adam alisema kuwa kamati yake inawaomba wapenda muziki wote nchini kwenda kupokea mwili wa msanii huyo mkali ya 'freestyle' pindi utakapowasili.

"Baada ya mwili huo kuwasili nchini, moja kwa moja utakwenda kuhifadhiwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na kesho Jumatano utaagwa katika viwanja vya Leaders Club na hatimaye safari ya kuupeleka mwili huo katika nyumba yake ya milele mkoani Morogoro itaanza," alisisitiza Adam.

Taarifa za kuletwa mwili huo nchini zilileta faraja kwa familia ya marehemu ambapo juzi msiba wa familia ulipo Mbezi eneo la Goigi, wanafamilia walionekana kusikitishwa na kuchelewa kufika mwili huo.

Juzi msemaji wa kamati hiyo, Adam Juma alitoa kauli ya kukata tamaa baada ya kuulizwa na gazeti hili kuwa ni lini mwili wa msanii huyo utawasili.

"Kwa kweli sina la kusema, mimi naona tuendelee kuvuta subira, mi' mwenyewe sielewi nashindwa hata kula....," alisema Adam.

Akizungumza na NIPASHE jana msanii wa siku nyingi wa muziki wa hiphop nchini na rafiki mkubwa wa marehemu, Jaymoe alisema kuwa angalau moyo umetulia baada ya kusikia kuwa mwili wa rafiki yake kipenzi utawasili nchini. "Ni furaha kwangu hata kwa familia yake haswa bi mkubwa wake (mama yake) kwani kule ni mbali nadhani baadhi ya watu ilifika kipindi walikata tamaa baada ya kuona siku zinakwenda na kule ni mbali....kamati ipo makini na mwili utakuja...".

Balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini, Radhia Msuya, ambaye amekuja nchini kwa ajili ya msiba huo na kwenda kuwatembelea wana familia jijini Dar es Salaam, alisema juzi kwamba kuchelewa kwa mwili huo kulisababishwa na taratibu tofauti za nchi hiyo katika kutoa kibali cha vifo.

Ngwair aliyekwenda nchini Afrika Kusini kufanya maonyesho, alifariki dunia usingizini nyumbani alipofikia huku msanii aliyeambatana naye akilazwa hospitalini huku sababu kilichowakuta kikiwa bado ni giza nene.

Balozi Msuya alisema vipimo vimeshatoka na vimekabidhiwa kwa familia ambayo itaamua kama ivitoe kwa umma ama isivitoe.  
 

0 comments:

Post a Comment

Blog Archive

Popular Posts

.

CHAT BOX

My Blog List

 
Support : BONGOCLANTZ
Copyright © 2013. KANGAROO - All Rights Reserved
Template Created by EDDIE SUCRE
Proudly powered by Blogger