Home » » CBE mabingwa pool vyuo vikuu taifa

CBE mabingwa pool vyuo vikuu taifa

Chuo cha Biashara (CBE) cha mkoa wa Dar es Salaam juzi kilitawazwa kuwa mabingwa wapya wa fainali za taifa za mashindano ya mchezo wa pool kwa wanafunzi wa vyuo vikuu nchini baada ya kuibuka na ushindi wa magoli 13-5 dhidi ya chuo cha Mzumbe cha mkoa wa Mbeya katika mechi ya fainali.

Fainali za mashindano hayo yanayojulikana kama 'Safari Lager Higher Learning Competition 2013' zilishirikisha vyuo vikuu vinane vilivyotwaa ubingwa katika ngazi ya mikoa. Bendi ya African Stars (Twanga Pepeta) ilitumbuiza fainali hizo zilizofanyika kwenye viwanja vya Leaders Club, Kinondoni jijini Dar es Salaam.

Chuo cha CBE kwa kutwaa ubingwa mashindano hayo yanayodhaminiwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kupitia bia ya Safari Lager, walijinyakulia fedha taslim Sh. milioni 2.5 na kikombe cha ubingwa.

Mzumbe (Mbeya) kwa kushika nafasi ya pili waliondoka na Sh. milioni 1.5, huku Mzumbe (Morogoro) walioshika nafasi ya tatu wakipata Sh. milioni 1.3. Chuo cha St. Augustine (Mwanza) kilizawadiwa Sh. milioni 1 kwa kushika nafasi ya nne.

Vyuo vikuu vya Rucco (Iringa), Muccobs (Kilimanjaro), IAA (Arusha) na St. John's (Dodoma) kila kimoja kilipewa kifuta jasho cha Sh.500,000 cha kushiriki fainali hizo.

Ubingwa wa mchezaji mmoja mmoja (wanaume) ulichukuliwa na Said Mohamed wa chuo cha Rucco aliyezawadiwa Sh.300,000, George Tito wa chuo cha Mzumbe (Morogoro) aliyeshika nafasi ya pili alipewa Sh.200,000 na Peter Patrick wa IFM aliyeshika nafasi ya tatu alipata Sh.150,000. Walter Thomson wa Mzumbe (Mbeya) alipewa Sh.100.000 kwa kushika nafasi ya nne.

Lilian Meory wa chuo cha CBE alitwaa ubingwa kwa mchezaji mmoja mmoja (wanawake) na kuzawadiwa Sh.200.000, Agnes Jacob wa chuo cha St. Augustine alishika nafasi ya pili na kuondoka na Sh.150,000, Amina Mhina wa Mzumbe (Mbeya) alishika nafasi ya tatu na kupewa Sh.100,000 na Lemi Jackson wa St.John's aliibuka katika nafasi ya nne na kupewa Sh.50.000.

Zawadi kwa washindi zilikabidhiwa na Mwenyekiti wa Baraza la Michezo Tanzania (BMT), Dionis Malinzi aliyekuwa mgeni rasmi katika fainali hizo.

0 comments:

Post a Comment

Blog Archive

Popular Posts

.

CHAT BOX

My Blog List

 
Support : BONGOCLANTZ
Copyright © 2013. KANGAROO - All Rights Reserved
Template Created by EDDIE SUCRE
Proudly powered by Blogger