Home » » Kibanda ana siri moyoni

Kibanda ana siri moyoni

Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) ambaye pia ni Mhariri Mtendaji wa New Habari (2006), Absalom Kibanda, akizungumza na waandishi wa habari katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa
Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Absalom Kibanda, amerejea nchini kutoka Afrika Kusini alikokwenda kutibiwa, huku akiwa na siri moyoni kuhusu kilicho nyuma ya matukio mabaya yaliyowasibu baadhi ya waandishi wa habari, akiwamo yeye, ambayo ameahidi kuisema iwapo Mungu atampa uzima.

Alisema atafanya hivyo ili kuliokoa taifa, wanahabari wenzake na Watanzania kwa jumla, ili kuwasaidia wasiingie kwenye madhila, maumivu na mateso kama yale yaliyompata.

Kibanda ambaye pia ni Mhariri Mtendaji wa Kampuni ya New Habari 2006 Limited, aliwasili nchini jana saa 7.55 mchana, akitokea Hospitali ya Milpark nchini humo, ambako alilazwa kwa miezi mitatu kisha kukaa hotelini kwa muda, baada ya kuvamiwa na watu wasiojulikana wakati akirejea nyumbani kwake, Mbezi Juu, jijini Dar es Salaam, Machi 5, mwaka huu.

Katika tukio hilo, watu hao walimng’oa meno, kumkata kidole, kumjeruhi kwa kitu kizito kichwani na kumharibu jicho la kushoto.

Baada ya tukio hilo, Machi 6, mwaka huu, Kibanda alilazwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) na baadaye katika Taasisi ya Tiba ya Mifupa (MOI), jijini Dar es Salaam.

Kisha  alipelekwa Afrika Kusini na kulazwa katika Hospitali ya Milpark, jijini Johannesburg.

Kibanda alisema hayo alipozungumza na waandishi wa habari muda mfupi baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) jijini Dar es Salaam jana na kupata mapokezi makubwa kutoka kwa mamia ya wakazi wa Dar es Salaam, wakiwamo wahariri, waandishi na wananchi wengine.

Alisema akiwa Afrika Kusini, alipata taarifa nyingi kuhusiana na tukio lake na mengine yaliyowasibu wanahabari wengine nchini.

Kibanda alisema hataki kufanya makosa ya watu wengine na kwamba, yeye mwenyewe anakusudia kuyasemea hayo kila wakati.

“Katika matukio yangu na mengine, kama Mungu atanipa uzima nitalisemea. Tumekuwa tukipata taarifa nyingi,” alisema Kibanda.

Alisema alipouawa mwandishi wa habari aliyekuwa mwakilishi wa kituo cha televisheni ya Channel Ten, mkoani Iringa, marehemu Daud Mwangosi, alishiriki katika kutoa tamko la TEF lililokuwa la pamoja na Baraza la Habari Tanzania (MCT).

Pia alishiriki katika kufuatilia matukio mbalimbali ya waandishi kuumizwa au kujeruhiwa, likiwamo lile lililomsibu Shaban Matutu (Tanzania Daima) na Mnaku Mbani (Business Times).
“Nataka kuwahakikishia wanahabari wenzangu, kwamba, matukio yote haya si ya bahati mbaya,” alisema Kibanda.

Alisema wakati akiyapitia na kuyaangalia matukio ya wanahabari wenzake, hakujua hata siku moja kwamba, pengine na yeye kama angefikwa na matukio hayo.

“Nawaomba wanahabari wenzangu tufanye lolote tunaloweza kuhakikisha tukio la Kibanda linakuwa la mwisho. Matukio ya watu kupanga njama au kula njama na kujeruhi watu,” alisema Kibanda.

Kibanda alisema tukio la kutekwa, kuteswa na kujeruhiwa kwa aliyekuwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari Tanzania, Dk. Stephen Ulimboka, linafanana sana kimazingira na kimkakati na tukio lake.

Kibanda alisema akiwa hospitali Afrika Kusini, serikali ilituma mpelelezi, ambaye ni afisa wa ngazi za juu wa Jeshi la Polisi kuzungumza naye juu ya janga lililomkuta.

Pia alisema hataki kabisa kuwa mbinafsi kwa sababu anajua kwamba, mpaka sasa wanahabari na Watanzania kwa jumla wanashuhudia ukimya miongoni mwa vyombo mbalimbali vya dola unaoendelea kuhusu hatima ya uchunguzi wa tukio lake.

Kibanda alisema kinyume cha ukimya huo, vyombo hivyo viliahidi kwamba, vitalifanyia kazi tukio lake kwa kina na hatimaye watu waliohusika kufikishwa mbele ya mkono wa sheria.

Alisema kabla hajaondoka hospitali, alitembelewa na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Inspekta Jenerali (IGP), Said Mwema, na Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Naibu Kamishna (ACP) Suleiman Kova.

Kwa mujibu wa Kibanda, ahadi ya kulifanyia kazi tukio lake alipewa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi, alipomtembelea hospitali Afrika Kusini, kwamba serikali itafanya lolote inaloweza.

“Bado namuuliza Mungu kwanini aliruhusu niwe hai hadi leo? Kama kuna ujumbe wa uhai wangu leo nina wajibu ninaotaka kuutimiza ili kuliokoa taifa langu, wanahabari wenzangu na Watanzania wengine wasiingie katika madhila, maumivu na mateso makali, ambayo nimepata,” alisema Kibanda.

Alisema ana kila sababu ya kufanya jambo, ambalo litawatoa Watanzania hapa walipo sasa.
“Kwa sababu hiyo nasema ndugu zangu, msimlilie Absalom Kibanda. Ililieni nchi yetu, ambayo katika kipindi cha miaka karibu nane ya utawala wa awamu nne, matukio ya namna hii yanaendelea kushamiri na hakuna linalofanyika,” alisema Kibanda.

Alisema akiwa Afrika Kusini, alisoma taarifa na kusikia kauli mbalimbali kutoka kwa wanasiasa, wanahabari na watu wengine kuhusu tukio lake.

Kibanda alisema la mwisho alilolisoma lilikuwa ni tamko la TEF, ambalo alisema walifanya kazi kubwa, ikiwa ni pamoja na kuandika muhtasari mzito sana.

Alisema zaidi ya hivyo, TEF walisafiri kwenda Afrika Kusini kuzungumza naye ingawa wakati huo alikuwa na maumivu makali kulinganisha na hivi sasa, lakini walifanikisha kazi yao na matokeo ameyaona.

Kibanda alisema: "Kama utasoma ripoti ya TEF, utagundua kwamba, kuna mambo mengi yaliyo nyuma ya ripoti hiyo."

Kabla ya kuanza kuzungumza hayo, Kibanda alibubujikwa machozi baada ya kushuhudia umati mkubwa wa watu waliofika uwanjani hapo kumpokea.

Baadhi wanahabari walibeba mabango yenye ujumbe wa kumkaribisha nyumbani na kuvihoji vyombo vya dola kuhusu hatima ya uchunguzi wa tukio lake.

Kibanda alisema ametoa machozi kwa sababu ya mshikamano mkubwa aliouona jana katika mapokezi yake.

Aliwashukuru wahariri, wanahabari, vyombo vyote vya habari na Watanzania kwa jumla kwa moyo wa ushirikiano na mshikamano waliouonyesha kufuatia matukio yaliyomsibu.

Pia alimshukuru Mwenyekiti wa Chama Wamiliki wa Vyombo vya Habari Tanzania (Moat), ambaye pia ni Mwenyekiti Mtendaji wa IPP, Dk. Reginald Mengi, kwa msaada mkubwa alioutoa kwake.

Alisema bado ana maumivu ya mwili, lakini hana maumivu ya roho na kuwaambia wanahabari na Watanzania kwamba, wana wajibu wa kuliokoa taifa kwani limepita katika kipindi kigumu.
 

0 comments:

Post a Comment

Blog Archive

Popular Posts

.

CHAT BOX

My Blog List

 
Support : BONGOCLANTZ
Copyright © 2013. KANGAROO - All Rights Reserved
Template Created by EDDIE SUCRE
Proudly powered by Blogger