Msemaji wa JWTZ, Kanali Kapambala Mgawe |
Taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Habari na Uhusiano Makao Makuu ya Jeshi hilo jijini Dar es Salaam jana, ilisema ujumbe huo unasema: ‘Habari zilizotufikia hivi punde.
Mtanzania yeyote kaa makini usiokote kitu chochote ambacho una shaka nacho, kuna mabomu yamerushwa toka nchi jirani ya Malawi zaidi ya 30 zenye uzito usiopungua tani 100. Hivyo basi uonapo kitu kipo kama chupa ya chai chenye rangi ya fedha, Usiguse’.
Pia ujumbe huo unaelekeza kuwa piga namba 0756 000042 na SMS hii tuma kwa watu uwezavyo. Imetolewa na JWTZ’.
Taarifa iliyotolewa na JWTZ imewaondoa hofu wananchi kuwa ujumbe huo ni uongo na kwamba haujatolewa na jeshi hilo.
“Kwanza, Ujumbe huo haujatolewa na JWTZ. JWTZ haliwezi likatumia mfumo huo wa SMS kuwapa wananchi taarifa za hatari kama hizo” ilisema taarifa hiyo.
Taarifa hiyo ilifafanua kuwa JWTZ hutangaza kupitia vyombo rasmi kama vile magazeti, radio na televisheni linapotaka kutoa taarifa kwa wananchi.
Pia taarifa hiyo ilisema kuwa bomu la tani 100 ni zito mno, halijawahi kutengenezwa duniani na kama lipo, haifahamiki bomu hilo litarushwa vipi , kwa kutumia ndege au mzinga.
"Lakini pia, mzinga wa aina hiyo haupo duniani kote na wala hakuna ndege yenye uwezo huo, hasa kwa bomu lenye umbile dogo kama hilo (Chupa ya Chai)," taarifa ilieleza na kuongeza:
"Tunawaomba wananchi wazipuuzie taarifa hizi kwani sio za kweli ni uongo mtupu. JWTZ lipo kwa ajili ya wananchi hivyo, kwa taarifa hizi za hatari lazima lingewajulisha kwa njia zilizoelezwa hapo juu na si kwa simu za mkononi."
CHANZO:
NIPASHE
0 comments:
Post a Comment